WILAYA DODOMA YAKABILIWA UHABA WA MBEGU - Rhevan Media

WILAYA DODOMA YAKABILIWA UHABA WA MBEGU

5264122426_baedb1a072_b



WILAYA ya Dodoma inakabiliwa na uhaba wa mbegu za mazao yanayostahamili ukame kama mtama, hali inayosababisha baadhi ya wafanyabiashara kufanya udanganyifu kwa kuuza mbegu feki.
Dodoma ni miongoni mwa mikoa yenye ukame ambayo wataalamu wa kilimo wamekuwa wakiwashauri wananchi kulima mazao yanayostahamili ukame kama vile mtama, uwele na mihogo, huku wananchi wakitahadharishwa kuwa makini wakati wa kununua mbegu.
Mkuu wa Ghala la Hifadhi ya Chakula Kanda ya Kati (NFRA), Hopf Mwakaje alisema mbegu za mtama kwa wilaya hiyo hazipatikani.
Wakizungumzia hali ya mvua hadi sasa, baadhi ya wakulima wamesema japokuwa wananchi wameandaa mashamba na wengi wao wameshapanda, bado mvua haiwapi matumaini ya kupata mavuno, kwani msimu wake umepita.
Mkulima mwingine, Anna Mng’ong’o, alisema hali ni mbaya kutokana na mbegu za mtama kutopatikana.
“Tunaomba Serikali itusaidie mbegu ya mtama na uwele kutokana na kuwapo uhaba mkubwa mbegu,” alisema.
Katibu Tawala wa Wilaya Dodoma, Jastina Mboneko, alisema chakula kipo cha kutosha na hakutakuwa na tatizo la njaa.
MTANZANIA ilitembelea soko kuu la Mazengo na kushuhudia uwapo wa vyakula vingi.
Mwenyekiti wa soko hilo, Godson Rugazama, alisema kumekuwapo na ongezeko la bei kutokana na wakulima kushindwa kutoa vyakula kwa wingi kwa hofu ya hali ya mvua.
Previous
Next Post »