ABOOD AMWAGA SH MILIONI 48 ZA ADA - Rhevan Media

ABOOD AMWAGA SH MILIONI 48 ZA ADA

 Tokeo la picha la ABOOD BOSI

MBUNGE wa Morogoro Mjini, Abdulaziz Abood (CCM), amekabidhi Sh milioni 48  kwa ajili ya kulipia ada wanafunzi wa elimu ya juu, shule za sekondari na shule za msingi waliopo ndani ya Manispaa ya Morogoro kwa kipindi cha Januari mwaka huu.
Makabidhiano hayo yalifanyika jana mjini hapa mbele ya wazazi, ambapo Abood alisema suala la elimu linapaswa kupewa kipaumbele kwa kuunga mkono jitihada zinazofanywa na wadau kwa kushirikiana na Serikali.
Alisema kuwa hakuna haja ya mzazi na mlezi kuacha ama kushindwa kumpeleka mwanae shule wakati Serikali iliondoa mfumo wa malipo kwa wanafunzi wa shule za msingi  na kuacha majukumu ya kununua sare, mahitaji mengine kwa wazazi na walezi.
“Mimi kama mzazi nimeamua kujinyima na familia yangu tuwapokee baadhi ya wazazi majukumu, maana hawa ni watoto na wengijne ni vijana wangu wanastahili kupata elimu bora, hakuna urithi mzuri kama kumpa mtoto elimu,” alisema Abood.
Alisema fedha alizotoa  ni kutokana na vyanzo vyake vya mapato huku akiwa amedhamiria kuimarisha elimu hasa kwa watoto, vijana wa jimbo lake kwa kuwasaidia wazazi sehemu ya majukumu yao.
Mbali na hilo mbunge huyo amekabidhi mbao zenye thamani ya Sh milioni 9.8 kwa ajili ya ukarabati wa Shule ya Msingi Kauzeni iliyoezuliwa na mvua kubwa iliyoambatana na upepo mwishoni mwa  mwaka jana.
Akizungumzia hatua hiyo mkazi wa Morogoro, Said Mkwinda alisifu jitihada zinazofanywa na mbunge huyo katika kuboresha sekta ya elimu pamoja na huduma mbalimbali jimboni humo.
“Hakuna mtu anayefika katika ofisi ya mbunge kuomba msaada ana kosa, Abood anatoa msaada kwa watu wote bila itikadi ya chama, dini wala kabila,huyu ndiyo kiongozi watu anapaswa kuungwa mkono katika kazi yake ya ubunge,” alisema.
Previous
Next Post »