Na Mwandishi Wetu
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeitaka Taasisi za Serikali na Mashirika yote ya Umma kutumia kituo cha kutunzia kumbukumbu cha Taifa (National Data Centre)chenye hadhi ya juu kabisa katika viwango vya ubora na usalama wa Taarifa na Kumbukumbu.
Kamati pia imezitaka Taasisi zote zilizo chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kutumia Kituo hicho katika kutunza kumbukumbu zake ili kuwa mfano kwa Taasisi nyingine za Umma.
Akizungumza katiko maazimio ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu mara baada ya ziara ya siku moja ya Kamati hiyo kuitembelea Kampuni ya Simu Tanzania TTCL pamoja na miradi ya Mkongo wa Taifa na Kituo Mahiri cha kutunzia kumbukumbu (Data Centre), Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mheshimiwa Norman Sigala amesema, uhai wa Kampuni ya Simu Tanzania TTCL upo mikononi mwa Serikali ambayo ina jukumu kubwa la kuihusiha Kampuni hiyo yenye uwekezaji mkubwa.
Aidha, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imezitaka Taasisi zote za Umma na binafsi kulipa madeni zinazodaiwa na TTCL kuiwezesha Kampuni hiyo kujiendesha kwa ufanisi ikiwa ni pamoja na Watendaji wa Umma wanaogharamiwa huduma za Mawasiliano kutumia huduma za simu za TTCL katika maeneo yote yenye huduma hizo.
Mjumbe wa Kamati hiyo Mhe Rita Kabati amesema, kukamilika kwa Mchakato wa kuondoka kwa Bharti Airtel ndani ya TTCL kunahitaji kwenda sambamba na uwezeshaji wa mtaji kama ilivyofanyika kwa Kampuni ya Reli Tanzania(TRL) na Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) ambazo sasa zinafanya vizuri.
Sign up here with your email
