PLUIJM AMUONYA LWANDAMINA - Rhevan Media

PLUIJM AMUONYA LWANDAMINA

Tokeo la picha la LWANDAMINABAADA ya uongozi wa Yanga kutangaza rasmi hapo jana kumkabidhi madaraka ya ukocha Mzambia George Lwandamina, na Hans-van-der-Pluijm kuwa Mkurugenzi wa Ufundi, Mholanzi huyo amemtahadharisha mwenzake kuwa haitakuwa kazi rahisi kutetea taji la ubingwa wa ligi bila ushirikiano.
HabariLeo lilifanya mazungumzo na Pluijm jana mchana kwenye Makao Makuu ya klabu ya Yanga, ambapo alikiri kukubaliana na uongozi wa Yanga kuwa katika nafasi ya Mkurugenzi wa Ufundi na kuahidi kumpa ushirikiano kocha mpya Lwandamina.
“Ni kweli nimekubali kuwa Mkurugenzi wa Ufundi na nina furaha kwa nafasi mpya. Niseme tu kuwa hii ilikuwa ni sehemu ya mkataba wangu wa miaka miwili niliosaini Juni mwaka huu, ilikuwa na vipengele viwili cha Ukocha na Ukurugenzi wa Ufundi kwa hiyo nimebaki na kimoja,” alisema.
Pluijm alisema baada ya kukabidhiwa jukumu jipya kitu cha kwanza anataka kukutana uso kwa uso na Lwandamina na kujadiliana nini cha kufanya kwa ajili ya kuboresha na kisha kuanza kazi rasmi.
Kocha huyu kwa kushirikiana na Lwandamina wanatarajia kuanza kazi rasmi Novemba 25 mwaka huu, ambapo wachezaji wataanza kurejea kwa ajili ya maandalizi ya mzunguko wa pili.
Pia, Kocha huyo wa zamani wa Yanga alisema hamfahamu vizuri Lwandamina, anachojua alikuwa ni Kocha wa Zesco United kutoka Zambia na kwamba yuko tayari kushirikiana naye.
Alisema lengo la kwanza ni kuhakikisha wanafanya kazi pamoja ili kutetea ubingwa, huku akisema kuwa hakuna kazi rahisi ni lazima washirikiane kuonesha kuwa wao ni Yanga wa ukweli.
“Ili kuwa bingwa ni lazima upitie changamoto nyingi, lakini muhimu ni kushirikiana na kupambana, kuhakikisha mnafanya vizuri,”alisema.
Pluijm hakusita kuzungumzia sababu za kukataa nafasi hiyo awali, akisema kuwa aliona kuwa yeye ni Kocha bora, amefanya vizuri katika ligi lakini pia, alifanya vizuri kwenye michezo ya kimataifa hivyo, alikuwa akijiuliza kwanini awe Mkurugenzi wa ufundi? Na sio kocha wakati bado ana uwezo.
Pia, alitoa sababu za kukubali nafasi hiyo kwa sasa, akisema kuwa anapenda mpira ni kazi yake, bado anahitaji kuisaidia timu hiyo kufanya vizuri zaidi. Kutakiwa Ghana Pluijm alipigiwa simu na vyombo vya habari vya Ghana mbele ya mwandishi wa gazeti hili, kuhusu tetesi za yeye kwenda kuifundisha timu ya taifa ya Ghana.
Gazeti hili lilipouliza kuhusu hilo alisema si vizuri kuzungumzia hayo, wakati bado ana mkataba na Yanga. Mbali na Ghana kumhitaji, pia anatakiwa na klabu ya Orlando Pirates ya Afrika Kusini ingawa anashindwa kuweka wazi. Alisema lolote linaweza kutokea wakati wowote, na yupo tayari kuendelea kuwa Kocha iwapo atahitajika kwa kuwa yupo imara, na ana uwezo.
Mikataba ya wachezaji Pluijm alisema atashirikiana na Lwandamina kufanya mazungumzo na wachezaji ambao mikataba yao inaelekea ukingoni, mara watakaporejea kutoka likizo kuona uwezekano wa kuwaongeza wale wenye uwezo na kwamba kila kitu kitakamilishwa kwa Kocha mpya.
Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Clement Sanga alisema awali kuwa, Pluijm alikubali kumkabidhi Lwandamina jukumu la ukocha na yeye kuwa Mkurugenzi wa Ufundi. Sanga alisema kuwa kocha huyo na mkurugenzi wa ufundi watatambulishwa wakati wowote wiki hii tayari kuanza kazi zao.
Previous
Next Post »