MBARONI KWA KUMPA MIMBA MWANAFUNZI - Rhevan Media

MBARONI KWA KUMPA MIMBA MWANAFUNZI


kamanda-andrew-satta.
MARA: Jeshi la Polisi Kituo cha Nyamongo, Kanda Maalum Tarime/ Rorya mkoani Mara, linamshikilia Wang’enyi Juma, 24, (pichani)mkazi wa Wilaya ya Serengeti, Mara akituhumiwa kumpa mimba mwanafunzi wa Shule ya Msingi Igogo jijini Mwanza (jina limehifadhiwa), mwenye umri wa miaka 16.
Taarifa zilizothibitishwa na polisi kanda maalum chini ya kamanda wake, ACP Andrew Satta zinasema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa hivi karibuni kisha kufunguliwa jalada la mashtaka namba NYM/ RB/1491/2016- Kumtia mimba mwanafunzi.
Taarifa zilizotolewa na afisa mmoja wa polisi aliyekataa kutaja jina lake kwa sababu si msemaji wa jeshi hilo, zinaeleza kuwa mtuhumiwa huyo baada ya kukamatwa, alihojiwa na polisi kituoni hapo na wakati wowote atapandishwa kizimbani.
“Mtuhumiwa huyo tulimkamata na tunatarajia kumpandisha mahakamani muda wowote kwa makosa  ya kumpa mimba mwanafunzi …(anamtaja jina),” alisema afisa huyo wa polisi.
Mwanafunzi aliyepewa mimba anasoma darasa la tano, alianza utoro na baadaye akaacha kabisa shule baada ya kudaiwa kurubuniwa na kijana huyo, wakawa wanaishi kama mume na mke.
Kaka wa mwanafunzi huyo aliyefahamika kwa jina moja la Mwita, alikuwa na haya ya kusema: “Huyu kijana alimtorosha mdogo wetu na kumfanya mke na kwamba hadi sasa hivi imebainika kwa mujibu wa vipimo vya hospitali, amempa ujauzito, ni lazima sheria ichukue mkondo wake.”
Mwandishi wetu aliona taarifa ya daktari iliyothibitisha kwamba mwanafunzi huyo ana ujauzito.
Previous
Next Post »