Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Amos Makalla amekumbana na joto la Mbeya baada ya
meya wa jiji hilo, Mchungaji David Mwashilindi na madiwani wake 34
kususia kikao chake cha kujitambulisha kwa wananchi, baada ya kudaiwa
kwenda kukagua Soko la Mwanjelwa bila kumpa taarifa yoyote meya wa jiji
hilo.
Meya alifikia uamuzi huo ndani ya ukumbi wa Mkapa muda
mfupi kabla ya Makalla kuanza kuzungumza na watumishi wa jiji, wananchi,
wazee maarufu, viongozi wa dini na machifu ambapo Mkuu wa Wilaya ya
Mbeya Nyirembe Sabi alimkaribisha Meya Mwashilindi kuzungumza chochote
kwa niaba ya madiwani wake.
Hata hivyo, Meya Mwashilindi
alipochukua kipaza sauti alisema: “Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, nakumbuka kwa
mara ya kwanza kukutana na wewe tulizungumza kwamba tufanye kazi, siasa
zimekwisha. Lakini masikitiko yangu ni kwamba leo hii umekwenda Soko la
Mwanjelwa bila ya mimi mwenye jiji kupewa taarifa yoyote wala madiwani
wangu. Sasa hiki kikao hakinihusu hivyo muendelee na kikao chenu.”
Baada
ya kusema maneno hayo alikabidhi kipaza sauti kwa mkuu wa wilaya, kisha
akachukua nyaraka zake akainuka pamoja na madiwani wote kupitia Chadema
na kutoka ukumbini huku wakisikika wakisema, ‘hizi ni siasa ambazo
tulizikataa, lakini wanatulazimisha kuendesha siasa. Hatuwezi kupuuzwa
kwa kiasi hiki.”
Sign up here with your email